Nalia napokumbuka, ifikapo siku yangu

Udongo tanifunika, tita liwe juu yangu

Siweze tena kutoka, nibakie peke yangu

Hiyo ndio siku yangu, tapoiaga dunia!


Kifikiria mauti, hutetema moyo wangu

Na ufikapo wakati, tauaga ulimwengu

Takoma zangu kunuti, swalati na dua zangu

Tanitoka roho yangu, tapoiaga dunia!


Nitaiaga dunia, nitengeke na wezangu

Sina tachokichukua, ila ni amali yangu

Hesabu yaningojea, sijui mezani yangu

Una hofu moyo wangu, tapoiaga dunia!


Nyumba iliyo nyembamba, takua makao yangu

Kiza kitachonikumba, kimbele ya macho yangu

Siwezi tena kuomba, ningoje hukumu yangu

Hako mtetezi wangu, tapoiaga dunia!


Aridhi ndio tandiko, takua malazi yangu

Hakuna taekuwako, atulize khofu yangu

Kwa hayo misukosuko, tahimili peke yangu

Tabakia peke yangu, tapoiaga dunia!


Wote watanikimbia, swahiba na watu wangu

Udongo nitolalia, takua ni mto wangu

Maringo yashanishia, sina tena cheo yangu

Takwisha ubosi wangu, tapoiaga dunia!


Takuwapi wa murua?, chaguo la moyo wangu

Naye atanikimbia, aniwache peke yangu

Vya ajabu tanijia, viumbe vya bwana Mungu

Wenye ya moto marungu, wajapo kunihujia!


Ya Rabi nijaalia, nifuzu hesabu yangu

Siku hiyo kiwadia, usamehe dhambi zangu

Pepo yako niridhia, iwe masikani yangu

Uniweke kwenye fungu, la waja wako radhia


Tamati tuikumbuke, siku hiyo ya matungu

Bure tusipumbazike, kwa raha za ulimwengu

Dini yetu tuishike, tumogope Bwana Mungu

Una kicho moyo wangu, tapoiaga dunia!


SWALEH SUHEIL ABEID

'Sauti Ya Haki'  Dubai - U.A.E.

Views: 96

Jibu Hii

Majibu ya Mjadala huu

Bismilahi Rahimi  Siku yenye ithibati

Kifo ni jambo azimi Isosomeka wakati

Si Suheli sio mimi   Kaumu yetu umati

KUONJA KWETU MAUTI- ALLAH AMETANGAZIA.

Kilio hakisimami   Unapofika wakati

Roho haijihami    Yake Maluki Mauti

Yoyote hamsakami Nguvu zilojizatiti

KUONJA KWETU MAUTI- ALLAH AMETANGAZIA.

Ewe Mja Yailahi     Uhai yako bahati

Kimbilia na kuwahi  Tumia wako wakati

Tenda yenye maslahi Yamridhio 'Al- Muqsiti'

KUONJA KWETU MAUTI- ALLAH AMETANGAZIA.

Tafakuri Ya Mauti   Hayataki hisabati

Jee, ushajizatiti     Kuyakabili mauti ?

Fikiri na kusukuti    Ufe ukawa hujuti

KUONJA KWETU MAUTI- ALLAH AMETANGAZIA.

Irabu niloiweka      Sisitizo ya Umati

Bora ujumbe kufika  Tusilie Yalaiti

Wajibu tukasikika     Kuliko kuwasaliti

KUONJA KWETU MAUTI- ALLAH AMETANGAZIA.

Babengwa hujakasiri, kweli zako kalimati

Kusema kwa ujasiri, siku yenye ithibati

Wajibu kuifikiri, ziwe njema hisabati

Daima tuyakumbuke, Mauti yatungojea

 

Hebu tuwe na fahamu, tuombe kila wakati

Siku hiyo ikitimu, hayakingiki mauti

Ghafula tu marehemu, kinga njema hesabati

Daima tuyakumbuke, Mauti yatungojea

 

Wako wapi makhuluki, katika wetu umati?

Walokua ni Maliki, wakwasi wenye dhuriyati

Mara wakitahamaki, wameshazikwa tiati !

Daima tuyakumbuke, Mauti yatungojea

 

 

yaweza kuwa shirki, mja kuhofu mauti,

ambayo hayamfiki, ila muda na wakati,

saa atapo fariki,yumo kwenye harakati,

ameshika guruneti,

jihadi mwendo mtundo!



mwendo mdundo jihadi, rijali kajidhatiti,

Amuitika munadi, wito kwenda jannati,

pale afapo shahidi, wallahi hiyo bahati!,

ameshika guruneti,

jihadi mwendo mdundo!


mara 'ti' 'parakacha', kalifyatuwa roketi,

hudumu bila kuwacha, hamsa yu swalawati,

anapo pambana kucha, roho yuko sakarati,

ameshika guruneti,

jihadi mwendo mdundo!


akipona "songa mbele!", anafata khutuwati,

hata kama kwa gobole, au jiwe la manati,

atapopigwa mshale, kuwa hoi, maututi,

ameshika guruneti,

jihadi mwendo mdundo!

ndipo huja malaika, kwa maelfu umati,

kuwa "ewe mtajika", nafsiyo mardhwati,

Peponi wahitajika, mafutuha lako geti,

una tele khairati,

leo furahi, uhondo!

Dikupa Dikupatile Dikilema (cheko lenye afya)

Kufa kwako kwa jihadi, kuondoa dhulumati

Kwa kifo cha ushahidi,  takujazi Jabaruti

Na ndio yake ahadi, una tele khairati

Utangia jan'nati, ufapo kwenye jihadi

 

Uwe safi wa fuadi, mwenye imani thabiti

Uwe kati ya junudi, ulipuwe guruneti

Uwe jasiri shadidi, usiogope mauti

Utangia jan'nati, ufapo kwenye jihadi

 

Sijifanye mujirimu, kuwalipua umati

Na kwajifunga mabomu, ufe kwa uafiriti

Ni kifo cha udhalimu, na thawabu huzipati!

Utangia jan'nati, ufapo kwenye jihadi

SWALEH SUHEIL ABEID  'Sauti Ya Haki'

RSS

© 2012   Created by zanzibarwebsite.com.

Lebo  |  Report an Issue  |  Terms of Service